Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Kimataifa la Ahlul-Bayt (AS) ABNA, Marjaa wa Kidini wa Iran, Ayatollah Hussein Nouri Hamedani, amesisitiza kuwa kipaumbele kikuu cha taifa kwa sasa ni kulinda umoja wa kitaifa na kuzuia migawanyiko katika jamii. Kauli hiyo ameitoa alipokutana na Mkuu wa Ofisi ya Rais wa Iran, Mohsen Haji Mirzaei, ambapo alitoa pongezi kwa juhudi za serikali katika kuhakikisha upatikanaji wa bidhaa muhimu wakati wa vita na kusisitiza umuhimu wa kuendelea kuwahudumia wananchi, kusimamia soko kwa umakini na kutatua changamoto za maisha ya watu.
Ayatollah Nouri Hamedani pia alieleza kuwa ni lazima kujibu ipasavyo uchokozi au uvamizi wowote wa adui ili kulinda heshima ya taifa na wananchi wake. Aidha, alionya dhidi ya kauli au vitendo vinavyoweza kusababisha mifarakano, akisisitiza kwamba hakuna anayepaswa kufanya jambo lolote linaloweza kudhoofisha mshikamano wa kitaifa.
Katika sehemu nyingine ya mazungumzo yake, alizungumzia nafasi maalumu ya mji wa Qom katika ulimwengu wa Kiislamu, akibainisha kuwa kutokana na hadhi yake ya kielimu na kidini, mji huo umekuwa kitovu cha kuvutia wanazuoni, viongozi na wageni kutoka mataifa mbalimbali ya Kiislamu. Hivyo, aliwataka viongozi kuupa umuhimu wa pekee mji huo na kuendelea kuunga mkono juhudi za maendeleo na ustawi wake.
Your Comment